Sunday, October 1, 2017

TANROADS IRINGA KUBORESHA BARABARA ILI WATALII WANUFAIKE



Na Mwandishi Maalum, IRINGA
Wakala wa barabara nchini (TANROADS) mkoa wa Iringa kuendelea kujenga na kuimarisha barabara ili watalii waweze kunufaika na huduma ya usafiri bora.

Kauli hiyo ilitolewa na msimamizi wa banda la TANROADS mkoa wa Iringa, Subira Anyisile alipokuwa akielezea nafasi ya TANROADS katika kukuza sekta ya utalii mkoa wa Iringa kwenye siku ya utalii duniani, maonesho ya utalii karibu kusini na shughuli za wajasiriamali wa viwanda vidogo - SIDO katika uwanja wa Kichangani mjini Iringa.
Msimamizi wa Banda la TANROADS


Anyisile alisema kuwa Wakala wa barabara una mchango mkubwa katika kukuza sekta ya utalii nchini. “Sisi TANROADS tunahusika na ujenzi na ukarabati wa barabara nchini. Utakubaliana nami kuwa barabara ndiyo kichocheo kikubwa cha kukuza sekta ya utalii nchini. Watalii hawawezi kufika mbugani au katika eneo la kivutio cha utalii bila barabara” alisema Anyisile. 

Katika kuhakikisha watalii wa ndani na nje wanaendelea kufurahia huduma za barabara, TANROADS imekuwa ikifanya ukarabati mkubwa na mdogo katika baadhi ya barabara zake ili zipitike muda wote. Alisema kuwa lengo la ujenzi na ukarabani wa barabara ni kurahisisha usafiri na kuchochea watalii kutembelea maeneo ya vivutio na kuuza na kununua bidhaa za kitalii. 

“Katika biashara hiyo mzunguko wa fedha unakuwepo na uchumi unakuwa kwa sababau maeneo mengi yanafunguka baada ya kuwa na mtandao wa barabara” alisema Anyisile.  

Akiongelea ujenzi wa barabara inayoelekea hifadhi ya Taifa ya Ruaha (Iringa- Msembe) kwa kiwango cha lami, Anyisile alisema kuwa upembuzi na usanifu umekamilika zinasubiriwa fedha tu.  
Wakala wa barabara mkoa wa Iringa unasimamia mtandao wa barabara wenye urefu wa km 1,192.9, kati ya hizo km 417.1 ni za lami na km 775.8 ni changarawe.
=30=

No comments:

Post a Comment