Friday, September 2, 2011


KARIBUNI KATIKA BLOG YA WANAFUNZI WOTE POPOTE TANZANIA (MATUKIO NA WANAVYUO)

Kwanza tunapenda kuwasalimu sana Ndugu walimu na wanafunzi na wadau wote mliopo popote nchini Tanzania na Duniani kwa ujumla, Kwa heshima na Taadhima tunapenda kuwatambukisha kwenu Blog mpya kabisa inayo kwenda kwa jina la MATUKIO NA WANAVYUO ambapo lengo kubwa ni kuwakutanisha wanavyuo wote Nchi nzima na kubadilishana mawazo pia kujua nini kinaendelea kila wakati kupitia mtandao huu, Hatuna mengi sana ya kuandika hapa kwa maana mtandao wenu unajieleza vizuri kabisa, pia mtandao huu ni wanavyuo wote waliopo vyuoni sasa na wale walio maliza pia ni wa watanzania wote kwa ujumla kwa maana kuna mambo yanayo wahusu na muhimu. Tunawaomba mpitie kila kona ya mtandao huu na kutoa maoni kama yapo nini kiongezwe ama kuboreshwa zaidi, Tunawakumbusha tena mtandao huu ni wako. sisi tunaongoza tuu kwa mawasiliano zaidi tutumie Barua pepe kupitia
( twanavyuo@live.com)
tunatanguliza  shukrani zetu pia atakae pata taarifa hii ampe na mwenzake
Asanteni sana.
Matukio na wanavyuo Crew

KUTEMBELEA MTANDAO HUU BOFYA HAPA
http://www.tzwanavyuo.blogspot.com/

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma,
Dkt. Christine Ishengoma


Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Dkt. Christine G. Ishengoma (Pichani)ameliagiza Jeshi la Polisi Mkoani Ruvuma kufanya ukaguzi wa kina katika magari yote yanayotumika kusafirisha abiria katika wilaya zote.
Katika agizo hilo, Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa, amesisitiza juu ya umuhimu wa kuyachunguza, kuyakagua na kuyazuia magari yote yenye hitilafu za kiufundi yasifanye kazi ya kusafirisha abiria na mizigo.
Lengo la agizo hilo ni kudhibiti matukio ya ajali ambazo zinaweza kugharimu maisha ya wananchi pindi ajali zinapotokea. Hii inafuatia tukio la hivi karibuni ambapo gari la abiria linalofanya shughuli zake kati ya Mbinga na Mbamba-bay kupata ajali na kusababisha vifo vya watu sita na wengine kujeruhiwa. Ajali hiyo ilitokea katika kijiji cha Chunya ikiihusisha gari lenye namba T.270 BDG.
Katika ajali hiyo, gari hilo lilikuwa limepakia abiria na mizigo miongoni mwake yalikuwa mafuta ya Diesel na Petrol, hivyo baada ya ajali kutokea, mafuta yalishika moto na kusababisha vifo hivyo.
Ili kutekeleza agizo hilo, Jeshi la Polisi Mkoa litatakiwa kukagua na kuwazuia wenye magari ya abiria kubeba mizigo ya mafuta ya diesel/petrol katika magari yao, kudhibiti na kuzuia gari kubeba abiria wengi zaidi ya uwezo wake na mwisho kuyazuia magari yote yasiyo na sifa na vigezo vya kubeba abiria kufanya hivyo kwa mujibu wa sheria ya usalama barabani.
Mwisho, Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa anatoa pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki wote waliopoteza ndugu zao kufuatia vifo hivyo na aidha, anawatakia pole na kuwafariji abiria wote waliojeruhiwa katika ajali hiyo na amesisitiza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wote waliosababisha ajali hiyo kutokea.
Imetolewa na:
Revocatus A. Kassimba,
Afisa Habari,
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa,
RUVUMA.


Wednesday, August 24, 2011

ZIARA YA MKE WA BALOZI WA MAREKANI MKOANI IRINGA KATIKA PICHA

Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma (kushoto) akiagana na
Meneja wa Hospitali ya Aga Khan-Iringa, Bibi. Veronica James (kulia) nje ya Ofisi
ya Mkuu wa Mkoa



Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma akibadilishana mawazo na Mke wa Balozi wa Marekani nchi Tanzania, Bibi. Jacquiline Lenhardf alipofika kumsalimia Kaimu Mkuu wa Mkoa Ofisi kwake

ZIARA YA MKE WA BALOZI WA MAREKANI MKOANI IRINGA KATIKA PICHA

Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma (kushoto),
Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Bibi. Gertrude Mpaka (kulia) na
Afisa USAID-Tanzania, Bibi. Ludovica Tarimo (katikati)
katika picha ya pamoja mj ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa

Friday, August 19, 2011

…WAHIMIZWA KULA VYAKULA VYA ASILI

Wananchi wa Nyanda za Juu Kusini wametakiwa kujenga utamaduni wa kula vyakula vya asili na kuachana na vyakula vya kisasa ili kujenga na kuboresha afya zao.

Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Sara Dumba (kulia) akila ugali wa mtama kwa mlenda na Mkuu wa Wilaya ya Ludewa Georgina Bundala (kushoto) akipata kikombe cha uji wa mtama katika kutoa hamasa ya ulaji wa vyakula vya asili.
Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Sarah Dumba wakati akihamasisha ulaji wa vyakula vya asili katika maonesho ya Wakulima na Wafugaji katika viwanja vya Johm Mwakangale, Uyole Mbeya.
Dumba amesema “nawahamasisha wananchi wote kujenga utamaduni wa kula vyakula vya asili ili kujenga na kulinda afya zao”.

Amesema ulaji wa vyakula vya asili unamfanya mtu kuwa na  nguvu na afya njema inayomfanya aweze kukabiliana na changamoto za kimaisha za kila siku na kutokuwa legelege.

Akiongea nje ya banda la maonesho la Halmashauri ya Wilaya ya Njombe, huku akiendelea kula ugali wa mtama kwa mlenda na simbilisi, Dumba amesema kuwa anajisikia furaha sana kwa sababu anapata “kitu roho inapenda” kwa sababu anapata mlo kamili.

Nae Mkuu wa Wilaya ya Ludewa, Georgina Bundala katika uhamasishaji huo amesema viongozi wanawajibu wa kuwahamasisha wananchi wanaowaongoza kwa mifano katika yale wanayoyahubiri.

Huku nae akiwa anapata kikombe cha uji wa mtama ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Njombe kwa ubunifu huo wa kuleta vyakula vya asili kwa uhamasishaji na si maneno matupu.

Amesema wananchi wa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini hususani mkoa wa Iringa wajenge utamaduni wa kulima zao la mtama ili kukabiliana na ukame unaotokana na mabadiliko ya hali ya hewa.
TANI MIL 1.4 ZAONGEZEKA MAZAO YA CHAKULA NA BIASHARA IRINGA
Mkoa wa Iringa umefanikiwa kuongeza kilimo cha mazao ya chakula na biashara hadi kufikia tani milioni 1.4 katika kipindi cha miaka 50 ya Uhuru.

Kaimu Katibu Tawala Msaidize, Sehemu ya Uchumi na Sekta za Uzalishaji, Shenal S. Nyoni akifafanua jambo

Akiwasilisha taarifa ya mafanikio ya kilimo katika miaka 50 ya Uhuru, Kaimu Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Uchumi na Sekta za Uzalishaji, Shenal Nyoni katika Iringa Day iliyofanyika katika ukumbi wa JKT ndani ya uwanja wa John Mwakangale Uyole, Mbeya yanapofanyika maonesho ya Nanenane Kanda ya Nyanda za Juu Kusini.

Nyoni amesema “katika miaka ya 60 mkoa ulikuwa ukizalisha tani laki 3.05 za mazao hayo na hadi kufikia mwaka 2011 mkoa umefanikiwa kizalisha tani milioni 1.4”.

Amesema katika sekta ya uvuvi mkoa una mabwawa 4,167 yanayozalisha tani 1,449 za Samaki na kuuingizia shilingi bilioni 4.3 kwa mwaka.
Nyoni amesema kuwa mkoa pia ulishiriki katika mashindano ya mifugo ya Afrika Mashariki na kuchukua nafasi ya kwanza. Katika mashindano hayo Halmashauri ya Wilaya ya Iringa ndiyo ilichukua ushindi huo.

Akiongelea sekta ya viwanda amesema mkoa una viwanda vya kusindika na kuyaongezea mazao thamani. Mkoa una viwanda vikubwa vinne, viwanda vya kati 53 na 66 ni viwanda vidogo na mashine 1,992 za kusaga nafaka.

Awali akitoa salamu zake Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma ambae pia ni Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma amesema kuwa mkoa wa Iringa umefanikiwa kuzalisha chakula cha kuutosheleza mkoa kwa sehemu kubwa na kuonesha masikito yake kwa baadhi ya sehemu zinazokabiliwa na upungufu wa chakula kutokana na upungufu mkubwa na ukame ulioyakabili baadhi ya maeneo hayo.

Amesema mkoa umalima mazao mengi yakimo mazao ya biashara kama mbao, chai, pareto, kahawa, alizeti na maua.

SUMBAWANGA YAPUNGUZA VIFO VYA AKINA MAMA

Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga imefanikiwa kupunguza idadi ya vifo vya akina mama hadi kufikia vifo 245 kati ya vizazi 100,000 mwaka 2010.

Hayo yamesemwa na Afisa Muuguzi wa Manispaa hiyo, A. Ngojo wakati akifafanua lengo namba mbili la Manispaa ya Sumbawanga la kupunguza vifo vya akina mama vitokanavyo na ujauzito katika maonesho ya nanenane yaliyofanyika katika viwanja vya John Mwakangale, Uyole- Mbeya.

Ngojo amesema kuwa hadi kufikia Disemba 2010 Manispaa ya Sumbawanga iliweza kufikia lengo kwa kupunguza vifo hiyo toka vifo 263 kati ya vizazi 100,000 mwaka 2008 hadi kufikia vifo 245 kati ya vizazi 100,000 Disemba, 2010.

Amezitaja hatua zilizofikiwa kuwa ni kutoa motisha kwa wakunga wa jadi wanaowapeleka wajawazito kujifungua kwenye vituo vya afya na kupata huduma za kitaalamu. Hatua nyingine ameitaja kuwa ni kuongeza watumishi wenye ujuzi kwenye vituo vya huduma za afya toka 61% kwa mwaka 2008 hadi 91% kwa mwaka 2010.

Vilevile, kuongeza huduma za mkoba za uzazi wa mpango kutoka vituo 7 kati ya 15 (47%) kwa mwaka 2008 hadi kufikia vituo 11 (73%). Pia kuihamasisha jamii kuhusu uzazi wa mpango na kuimarisha huduma za vifaa ikiwa ni pamoja na magari ya kubeba wagonjwa.

Aidha, Manispaa hiyo imefanikiwa kupunguza vifo vya watoto wa umri chini ya mwaka mmoja kutoka 37 kati ya watoto 1000 mwaka 2008 hadi 17 kati ya watoto 1000 kufikia Disemba 2010.


Wednesday, July 27, 2011

WATUMISHI WA RAS IRINGA WAPEWA SOMO LA RUSHWA 

Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa ilianzisha Mkakati wa kudhibiti Rushwa mahali pa kazi ili Ofisi hiyo iwe ni eneo salama kutolea huduma kwa wananchi.
Paulos Lekamoi, Mwanasheria wa Sekretarieti ya Mkoa wa Iringa


Hayo yamesemwa na Mwanansheria wa Ofisi hiyo, Paulos Lekamoi wakati akiwasilisha mada juu ya Sheria ya Rushwa na Wajibu wa Watumishi wa Umma katika kudhibiti vitendo vya rushwa katika ukumbi wa Chuo kikuu Huria Tanzania tawi la Iringa katika Manispaa ya Iringa.

Lekamoi amesema “katika kuhakikisha rushwa mahali pa kazi haina nafasi ilianzisha mkakati wa kudhibiti rushwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa”.

Amesema mkakati huo umezingatia mkakati wa kitaifa wa kudhibiti rushwa ambapo lengo kuu ni kuimarisha njia za kupambana na rushwa, kuweka mifumo ya uadilifu, uwajibikaji na uwazi katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa pamoja na uzingatiaji wa Sheria ya Rushwa ya mwaka 2007.

Lekamoi amesema katika sehemu ya III ya Sheria Na. 11 imeleta mabadiliko makubwa sana yanayoenda sambamba na Azimio la Umoja wa Mataifa la Mwaka 2005. Amesema Sheria hii imeongeza makosa yaliyopo kwenye Sura ya 329 ya Sheria kama ilivyorekebishwa Mwaka 2000 na kuyataja baadhi ya makosa kuwa ni mchakato wa rushwa (kifungu cha 4), kutumia nyaraka mbalimbali kumpotosha msimamizi (kifungu cha 6), Maafisa wa Serikali kutumia madaraka yao kujinufaisha (kifungu cha 7), kupatikana na mali yoyote ambayo imepatikana kwa njia ya Rushwa (kifungu cha 10).

Amesema kifungu cha 15 (i) (a) na (b) cha Sheria Na. 11, 2007 kinazungunzia makosa yanayohusu upokeaji wa rushwa ambapo Mtumishi wa Umma anaweza kujikuta amejiingiza aidha kwa kujua au kwa kutojua.

Ameyataja makosa hayo kuwa ni kushirikiana na mtu mwingine au mtumishi mwenyewe kushawishi kupokea au kukubalikupokea chochote kwa manufaa yake ili kutekeleza lengo lolote ambalo kimsingi anatakiwa alifanye katika shughuli zake za kila siku.

Vilevile, kifungu Na. 15 (a) kinamtia hatiani mtu yeyote atakaetoa ahadi ya kumpendelea mtu yeyote.


Zaidi ya asilimia 70 ya matumizi ya kawaida ya Serikali ni kwa ununuzi wa bidhaa, huduma na malipo kwa kazi za ujenzi wa miundombinu.

Akiwasilisha mada juu ya Sheria ya Manunuzi ya mwaka 2004, Uwezo wa Bajeti katika kufanikisha Manunuzi na Udhibiti wa Rushwa katika Manunuzi, Afisa Ugavi Msaidizi Mkoa wa Iringa, Janeth Kitinye amesema kuwa eneo la Manunuzi ya Umma ni muhimu sana kwa sababu hutumia sehemu kubwa ya fedha za walipa kodi wa Tanzania.

Bi. Janeth Kitinye, Afisa Ugavi Msaidizi Sekretarieti ya Mkoa wa Iringa akiwasilisha mada

Aidha, ufanisi katika eneo hili ni chachu ya kufikia baadhi ya malengo makubwa ya kiuchumi na kijamii ya Taifa.

Amesema kuwa ukiondoa mishahara ya watumishi wa Serikali, karibu asilimia 70 ya Matumizi ya kawaida ya Serikali ni Ununuzi wa bidhaa, huduma na malipo kwa kazi mbalimbali. Vilevile, amesema karibu asilimia 100 ya matumizi ya Maendeleo ni kwa ajili ya ununuzi wa bidhaa, huduma na malipo kwa ajili ya kazi za ujenzi wa miudombinu na miradi mingine ya Maendeleo.

Amewataka watumishi wa Umma kuona kuwa wanalo jukumu kubwa la kuhakikisha Manunuzi wanayoyafanya yanawawezesha kupata bidhaa na huduma zenye Ubora kulingana na thamani ya fedha zilizotumika.

Kitinye amesema Sheria ya Manunuzi ya Umma ya Mwaka 2004, na Kanuni zake za Mwaka 2005 kwa pamoja zinaweka misingi na taratibu za kweza kufikia adhima hiyo.

Ameongoza kuwa Vitengo vya Manunuzi Vinajukumu la msingi la kuhakikisha kuwa huduma muhimu zinawafikia watumishi wa Umma na Wahitaji wengine katika muda uliopangwa na katika ubora unaokubalika. Sharia ya Manunuzi ya Mwaka 2004 na Kanuni zake za Mwaka 2005 zinawapngoza Watumishi wa Umma katika misingi ya Utawala Bora na uwajibikaji kwa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.

Thursday, June 9, 2011

MKOA WA IRINGA WAIBUKA MSHINDI WA USAFI NA MAZINGIRA

Mkoa wa Iringa umepongezwa kwa kuibuka mshindi wa jumla katika mashindno ya afya na usafi wa mazingira nchini na kupata zawadi ya kombe na kutakiwa mikoa mingine kuiga mfano huo ili mikoa yote iwe na mazingira safi na salama.
Hayo yamesemwa na mgeni rasmi, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania , Mhe. Mizengo Pinda katika utoaji zawadi kwa washindi wa shindano la afya na usafi wa mazingira, aliyewakilishwa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Prof. Anna Kajumulo Tibaijuka  kwenye kilele cha maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani kitaifa yaliyofanyika mjini Songea.
Katika mashindano hayo ya afya na usafi wa mazingira yaliyoratibiwa na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Halmashauri za Manispaa (Iringa), Mji (Njombe) na Wilaya (Njombe) zimekuwa mshindi wa tatu (Manispaa ya Iringa), wa pili (Mji Njombe), na wa kwanza (Wilaya ya Njombe) katika ngazi ya Halmashauri za Manispaa, Miji na Wilaya.
Kitaifa Halmashauri ya Jiji la Mwanza ndiyo mshindi kati ya majiji matatu yaliyoshindanishwa. Kwa upande wa Halmashauri za Manispaa jumla ya Manispaa 17 zilishindanishwa na Manispaa ya Moshi iliibuka msindi ikifuatiwa na Arusha na Iringa. Upande wa Halmashauri za Miji jumla ya Halmashauri sita zilishindanishwa na Mpanda iliibuka mshindi ikifuatiwa na Njombe. Halmashauri ya Wilaya ya Njombe ilizishinda Halmashauri za Meru (namba mbili) na Rungwe (namba tatu). 
Mkoa wa Iringa umeibuka mshindi wa jumla wa mashindano ya Afya na Usafi wa Mazingira baada ya Halmashauri zake tatu za Iringa, Mji Njombe na Wilaya ya Njombe kushinda katika nafasi tofauti.
Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani huadhimishwa kitaifa kila mwaka tarehe 5 Juni na mwaka huu yameongozwa na kaulimbiu isemayo ‘panda miti na kuitunza: hifadhi mazingira’ mkoani Ruvuma katika Manispaa ya Songea. Maadhimisho haya kimataifa yamefanyika katika miji ya Delhi na Mumbai nchini India.
JENGENI UTAMADUNI WA KUPANDA MITI
Watanzania wametakiwa kuachana na utamaduni wa kupanda miti kwa mazoea hasa katika kipindi cha Maadhimisho ya Siku ya Mazingira kitaifa na kujenga utamaduni kwa kupanda miti mara kwa mara ili kujihakikishia mazingira salama ya kuishi.
Rai hiyo imetolewa na Prof. Anna Kajumulo Tibaijuka katika hotuba ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mizengo Pinda alipomuwakilisha kwenye kilele cha Maadhimisho ya wiki ya Mazingira Duniani yaliyofanyika kitaifa katika Mkoa wa Ruvuma, manispaa ya Songea.
Prof. Tibaijuka amesema “kupanda miti si fasheni bali ni kazi ya kudumu” hivyo utamaduni wa kupanda miti katika siku za maadhimisho hauna budi kuachwa na kufanya upandaji miti kuwa ni zoezi endelevu.  Amesema mazingira ni sehemu ya maisha ya binadamu na uhai hivyo utunzaji wake ni jambo la lazima kwa kizazi hiki ili kijacho kiweze kujivunia hazina hiyo.
Amesema maadhimisho haya yanaongozwa na kaulimbiu isemayo ‘panda miti na kuitunza ili kuhifadhi mazingira’. Kaulimbiu inawataka watanzania kukaa chini na kutafakari na kujipima kama hatua zinazostahili zimechukuliwa katika kulinda.
Aidha, amesema kuwa misitu husaidia sana upatikanaji wa mvua jambo linalotegemewa sana katika kilimo na shughuli nyingine za kijamii. Vilevile, amekemea tabia inayoendelea kukua ya utakaji miti na uchomaji wa mioto ovyo. Amesema “kupanda miti si kuboresha mazingira tu bali na kuongeza kipato tukokana na mazao ya misitu”.
Awali katika utangulizi wake, Dkt.  Terezya  Huvisa, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais-Mazingira amesema kuwa Serikali kupitia Wizara yake imeandaa mkakati wa kuhifadhi mazingira uliojikita katika kuielimisha na kuihamasisha jamii juu ya umuhimu wa mazingira na uhifadhi wa uoto wa asili.
Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani ni matokeo ya azimio la umoja wa Mataifa la mwaka 1972, la Stockhorm –Sweden na kitaifa yalizinduliwa tarehe 1 Juni, 2011 katika kiwanja cha Majimaji kilichopo Manispaa na Makamu wa Rais, Dkt. Mohamed Gharib Bilal. Maadhimisho yaha yamekwenda sambamba na maadhimisho ya miaka 50 ya Uhuri wa Tanzania na miaka 47 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar uliozaa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.


BAJETI YAUJENZI WA VIWANJA VYA MICHEZO IRINGA

Halmashauri za Mkoa wa Iringa zimeshauriwa kutenga bajeti ya kutosha ya kuhudumia michezo hasa ujenzi wa viwanja vya michezo ili kukabiliana na tatizo la upungufu wa viwanja hivyo.
Ushauri huo umetolewa na George Lukindo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji Njombe, wakati akifungua rasmi mashindano ya Umoja wa Michezo na Sanaa Sekondari Tanzania (UMISSETA) ngazi ya Mkoa yatakayopelekea kuundwa kwa timu ya UMISSETA ya Mkoa wa Iringa.
Lukindo amesema “upungufu wa viwanja vya michezo ni tatizo katika Mkoa wa Iringa kutokana na jiografia ya Mkoa wenyewe kutokuwa na maeneo mengi tambalale hivyo nazishauri Halmashauri za Mkoa huu zipange bajeti ya kutosha kwa shule kadhaa ili kujenga viwanja vya michezo”. Amesema huwezi kuongelea kuinua sekta ya michezo katika ngazi yoyote kama hutakuwa na viwanja vya kutosha na vilivyo katika ubora unaostahili kwa michezo husika.
Akiongelea ufinyu wa bajeti ya michezo ya UMISSETA, Lukindo amezishauri Halmashauri kuangalia uwezekano wa kuongeza fedha za ziada ili kufidia upungufu unaojitokeza.
Akisisitiza suala la nidhamu amesema mchezaji asiye na nidhamu UMISSETA si mahali pake. Amesema “mchezaji asiye na nidhamu hata kama atakuwa ni mzuri kiasi gani asiingizwe katika timu ya Mkoa”.
Wakati akimkaribisha mgeni rasmi kufungua mashindano ya UMISSETA, Mwenyekiti wa UMISSETA Mkoa wa Iringa ambae pia ni Afisa Elimu Mkoa, Joseph Mnyikambi amesema kuwa michezo ni upendo, furaha na msikamano na kusisitiza kuwa katika kipindi chote cha mashindano hayo suala la nidhamu lipewe umuhimu wa pekee. Vilevile, amewaasa wanamichezo kuwa wanapokuwa uwanjani lazima watarajie na kukubali kushinda, kutoka sare au kushindwa.
Katika risala iliyoandaliwa na UMISSETA Mkoa na kusomwa na Upendo Mdzovela iliainisha changamoto zinazoikabili michezo ya UMISSETA kuwa ni pamoja ufinyu wa bajeti inayotengwa na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi. Aidha, changamoto nyingine ni upungufu wa walimu wenye taaluma ya michezo na vifaa vya michezo na upungufu wa viwanja vya michezo.
Mechi za ufunguzi zilizofana sana kwa kuzishindanisha timu za mpira wa miguu ya Halmashauri ya Mji Njombe wasiosikia (viziwi) na timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa ambapo Ludewa waliibuka kidedea kwa ushindi wa 1-0. Katika mechi nyingine ya mpira wa pete timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa iliibwaga timu ya Wasiosikia ya Halmashauri ya Mji Njombe kwa mabao 7-3.
MAAFISA MICHEZO LAZIMA MUONEKANE

Maafisa Michezo wa Halmashauri wametakiwa kutoka na kushiriki katika shughuli zote za michezo katika Halmashauri zao ili kudhihirisha uwepo wao na kuinua kiwango cha michezo katika Mkoa wa Iringa.
Agizo hilo limetolewa na Kenneth Komba, Afisa Michezo Mkoa wa Iringa, wakati akizungumza katika kikao maalumu cha kuweka mikakati ya kufanikisha michezo ya Umoja wa Michezo na Sanaa Sekondari (UMISSETA) mkoani hapa kilichowakutanisha Wakuu wa Shule za Sekondari, Maafisa Elimu Taaluma Sekondari, Walimu wa Michezo na Afisa Michezo Mkoa muda mfupi baada ya kuzipokea timu za michezo mbalimbali ya UMISSETA kutoka katika Halmashauri nane za Mkoa wa Iringa uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa shule ya sekondari ya Mpeche Wilayani Njombe.  
Komba amesema ili kuimarisha michezo yote katika Mkoa wa Iringa “ni lazima Maafisa Michezo wa Halmashauri watoke na kushiriki katika shughuli za michezo katika Halmashauri kwa kushirikiana na wadau wengine wa michezo kwa sababu nyie ndio wataalamu katika tasmia ya michezo”. Aidha, amesisitiza ushirikishwaji wa Maafisa Michezo hao katika shughuli za michezo ili jamii iweze kunufaika na taaluma yao.
Komba ambaye pia ni Meneja wa timu ya UMISSETA ya Mkoa aliushukuru uongozi wa Umoja wa Wakuu wa Shule za Sekondari (TAHOSSA) ngazi ya Wilaya na Mkoa kwa kujipanga na kufanikisha kuanza kwa mashindano ya UMISSETA mkoani hapa. Amesema kuwa TAHOSSA wamefanikisha kuanza kwa mashindano hayo kutokana na nguvu waliyonayo iliyojengeka katika misingi madhubuti ya umoja wao na kuheshimiana. Amesema jambo lolote la kimichezo haliwezi kukwama kwa namna yoyote ile hasa likiwa ni shirikishi kwa wadau na likifanyika kwa moyo wa umoja na mshikamano mkubwa.
Mwenyekiti wa TAHOSSA Mkoa wa Iringa, Andrew Kauta, amewataka walimu wote kusimamia kwa dhati suala la nidhamu kwa wanamichezo wote pasipo kujali mipaka ya Halmashauri au Wilaya zao na kusisitiza kuwa katika nidhamu hakuna mipaka. Aidha, amesisitiza kuwa michezo ni umoja, mshikamano na burudani hasa suala la nidhamu likidhibitiwa zaidi katika mavazi na matumizi ya lugha.
Vilevile, amewata walimu wa michezo kuwasilisha takwimu sahihi za wanamichezo na michezo wanayoshiriki kwa kila Halmashauri ili kuondokana na upotoshaji wa takwimu na usalama wa wanamichezo.
Lengo la msingi la mashindano haya ya UMISSETA ngazi ya Mkoa ni kushindanisha Wilaya sita na Halmashauri zake nane za Mkoa wa Iringa na hatimaye kupata timu moja ya Mkoa itakayokwenda kushiriki mashindano ya Kanda yanayotarajia kutimua vumbi Mkoani Ruvuma kuanzia tarehe 2 Juni, 2011.
Michezo ya UMISSETA inatarajia kuanza leo ngazi ya Mkoa katika Wilaya ya Njombe na inatarajia kushirikisha jumla ya wanamichezo 1088 katika michezo mbalimbali. 
KILIMO CHA MTAMA KIIMARISHWE

Viongozi wa Mkoa wa Iringa wameshauriwa kuweka juhudi za dhati katika kilimo cha mtama ili kukabiliana na baa la njaa linayoyakabili baadhi ya maeneo katika Wilaya za Iringa na Kilolo mkoani hapa.
Ushauri huo umetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Mpwapwa, Darry Rwegasira wakati akitoa uzoefu wa jinsi Wilaya ya Mpwapwa ilivyofanikiwa katika kilimo cha mtama na kukabiliana na baa la njaa.
Rwegasira amesema mapokeo ya viongozi ni jambo la msingi sana katika kufanikisha kilomo cha zao la mtama. Kwa upande wa Wilaya yake amesema “mapokeo ya viongozi wa Wilaya ya Mpwapwa ni mazuri sana”. Amesema Wilayani kwake kuanzia Mkuu wa Wilaya, Madiwani, Afisa Kilimo, Katibu wa CCM na Maafisa Watendaji wanalima zao la mtama jambo linalowafanya wananchi kuona mfano na umuhimu wa kilimo hicho kutoka kwa viongozi wao.
Mkuu wa Wilaya amesema kuwa Wilaya ilitengeneza sheria mdogondogo zinazosimamia utekelezaji wa mkakati wa kilimo cha mtama Wilayani hapo. Aidha, alishauri kuwa nguvu kupindukia zisitumike badala yake uhamasishaji na elimu ndio msingi pekee wa kuwafanya wananchi kukubaliana na kilimo hicho na kwa kuangalia mifano kutoka kwa viongozi wao.
Vilevile, mkakati mwingine uliotumika ulikuwa ni uundaji wa timu na kamati kuanzia ngazi za kijiji hadi Wilaya zikiwahusisha wataalamu wa kilimo na viongozi.
Wilaya ya Mpwapwa ilichagua kata tisa za mfano na kila kijiji kilikuwa na wakulima 98 wanaotumika kama walimu wa kuwaelimisha wenzao.
Nae kiongozi wa timu iliyokwenda kujifunza kilimo cha mtama Wilayani Mpwapwa, Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Asseri Msangi, amewashauri wakulima wa Wilaya ya Mpwapwa kutumza ardhi vizuri dhidi ya uharibifu unaotokana na mmea uitwao kidua. Amesema kutokana na hatari yam mea huo kwa ardhi na mazao Serikali ya kikoloni ilitunga Sheria ya 1946 kwa ajili ya kulinda ardhi dhidi ya kuharibika. Msangi amesema “tunzeni ardhi yenu vizuri, ardhi ni mali msipoitunza mtaumbuka”, “msipoitunza ikaharibika mtaenda wapi kwingine tumejaa”. Vilevile, amewashauri wataalamu wa kilimo kuwa watu wanaopenda mabadiliko na kwenda na wakati katika kuboresha na kuinua kilimo.