Friday, May 25, 2012


UKUAJI WA UCHUMI UZINGATIE UHIFADHI WA MAZINGIRA
IRINGA

Serikali imeihimiza dhana ya ukuaji wa uchumi kuzingatia matumizi endelevu ya rasilimali yasiyoathiri mazingira kwa kuzingatia athari za muda za muda mrefu kwa mazingira kwa faida ya vizazi vijavyo.

Kauli hiyo imetolewa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Mohamed Gharib Bilal alipokuwa akihutubia uzinduzi wa jukwaa la uchumi wa kijani uliofanyika katika ukumbi wa St. Dominic mjini Iringa.

Dkt. Bilal amesema “matumizi yasiyo endelevu ya rasilimali hauna manufaa katika dunia ya leo. Watu wanapaswa kuachana na mbinu za kizamani za ukuaji wa uchumi wa matumizi shinikizi ya rasilimali, ambapo maendeleo yamekuwa yakigharimu mazingira; badala yake, wanapaswa kufuata mbinu mpya ambazo tija huongezwa kwa kutumia na kusimamia maliasili kwa ufanisi zaidi”.

Amesema kuwa shughuli za kujiletea uchumi lazima ziangalie kwa makini athari za muda mrefu kwa mazingira na haja ya kuhifadhi urithi wa nchi kwa manufaa ya vizazi kilichopo na vizazi vijavyo. Amesema kuwa uchumi wa kijani ni muhimu kwa sababu huchochea ukuaji wa uchumi, mapato na ajira. Amesisitiza kuwa hii ndiyo aina ya uchumi inayoleta maendeleo ya kiuchumi ya muda mrefu na yanayotoa fursa kwa wananchi wengi.

Makamu wa Rais amesema kuwa katika sekta mbalimbali kama kilimo, ujenzi, misitu na usafiri, uchumi wa kijani ndio uchumi unaotengeneza ajira nyingi kuliko ajira zilizopo katika hali ya kawaida. Ametolea mfano wa sekta ya uvuvi, “uchumi wa kijani utalazimisha kushuka kwa mapato na ajira katika muda mfupi na wa kati ili kujazia hifadhi asilia, lakini hali hii hubakia ya muda mfupi na baadaye sekta hukua na kutoa tija kubwa wananchi”.

Dkt. Bilal amesema kuwa ili jitihada za maendeleo ziweze kufanikiwa nchini, lazima zielekezwe katika uhalisia wa mambo. Amesema “zaidi ya asilimia 75 ya wananchi wan chi hii huishi vijijini. Hivyo, jitihada madhubuti za kupunguza umasikini na kuleta maendeleo lazima zilenge wakazi na uchumi wa vijijini ili kuwa na matokeo mazuri”.

Amesema kuwa upo uhusiano mkubwa wa wananchi masikini wa vijijini na mazingira yao kwa sababu huishi karibu na mazingira ya asili na hutegemea rasilimali za ardhi, maji na misitu kwa maisha yao.

Katika salamu za Mkoa wa Iringa zilizotolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma amesema kuwa zoezi la kupanda miti na kuhakikisha inatunzwa ni mkakati shirikishi unaowashirikisha wananchi na taasisi mbalimbali. Kila Halmashauri inazingatia agizo la serikali la kuwa na uzalishaji wa miche ya miti kwenye vitalu vyake isiyopungua miche 1,500,000 kila msimu. Amesema kwa miaka mitano iliyopita Mkoauliweka malengo ya kupanda miti 197,910,000 na kufanikiwa kupanda miti 266,871,064.

Akiziainisha changamoto zinazokwamisha juhudi za kutunza na kuhifadhi mazingira amezitaja kuwa ni uchomaji moto ovyo, ukataji miti ovyo bila kufuata kanuni na kulima kwenye vyanzo vya maji na miteremko mikali.

Jukwaa la uchumi la kijani linaratibiwa na taasisi ya Uongozi kwa lengo la kuwa na uchumi endelevu nchini.
=30=

WAFANYAKAZI WATAKIWA KUFANYA KAZI KWA JUHUDI 

MUFINDI
Serikali Mkoani Iringa imewataka Wafanyakazi Mkoani hapa kufanya kazi kwa juhudi, maarifa na nidhamu ili kujiletea maendeleo katika kazi.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma katika hotuba yake ya Siku ya Wafanyakazi Duniani iliyofanyika katika ngazi ya Mkoa Wilayani Mufindi.

Dkt. Christine amesema ili mfanyakazi yeyote aweze kuheshimika katika jamii, inampasa kuelewa umuhimu wa nafasi yake katika jamii, kwa kufanya kazi kwa juhudi, maarifa na nidhamu na kujituma kazini kwake, bila ya kufuatwafuatwa”. Kwa waajiri amesema “mwajiri anao wajibu mkubwa wa kutoa vitendea kazi bora, kujali usalama wa wafanyakazi na kutoa ushirikiano wa kutosha kwa wafanyakazi wake”.

Akiongelea wajibu wa vyama vya wafanyakazi, Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa vyama hivyo vinawajibika kuwaelimisha wananchama wao ambao ni watumishi wa Serikali, taasisi, mashirika mbalimbali, wafanyakazi wa hoteli na wafanyakazi wengine juu ya kuheshimu nafasi waliopewa katika jamii na kuelewa msingi wa ufanyakazi bora wa umma. Amesema miongoni mwa wajibu huo ni kuelimisha juu ya sheria, taratibu na kanuni za kazi, kufanya kazi kwa hekima na uadilifu, kuheshimu maadili na taaluma, kutunza siri za serikali, kutekeleza wajibu wake kama wafanyakazi,pasipo upendeleo.

Akiongelea kero dhidi ya wafanyakazi, Dkt. Christine amesema kuwa serikali imeendelea kutatua kero nyingi zinazowakalibi wafanyazi katika utendaji kazi wao. Amesema “hapo awali kulikuwepo kero nyingi zinazohusu wafanyakazi, kama vile ucheleweshaji wa mishahara, ucheleweshaji wa malipo kwa wastaafu, kero ya kutopata mikopo kwenye benki”. Amesema kuwa hali hiyo kwa sasa imerekebishwa na wafanyakazi ni mashahidi. Aidha, amekiri kuwa maboresho haya hayajafikia kiwango cha asilimia mia moja.

Akiongelea Sensa ya watu na makazi, Dkt. Christine amewataka wafanyakazi wote kushiriki kutoa taarifa na elimu kwa wananchi dhidi ya sensa ya watu na makazi itakayofaanyika tarehe 26 Agosti, 2012. amesema kuwa lengo la Sensa hii ni kupata idadi ya watu wote katika nchi, kwa umri na jinsi, mahali wanapoishi, hali yao ya elimu, hali ya ajira, hali ya vizazi na vifo na hali ya makazi. Amesema sensa hiyo ni muhimu sana kwa sababu inalenga kutathmini utekelezaji wa mipango ya maendeleo ya Mkakati wa Kupunguza Umasikini na kukuza Uchumi Tanzania (MKUKUTA) na mpango wa Kupunguza Umasikini Zanzibar (MKUZA). Napenda kuwahamasisha wananchi wote kujitokeza kwa wingi na kutoa taarifa zao kwa usahihi ili kufanikisha zoezi hilo.

Maadhimisho ya siku ya wafanyakazi duniani yalianza katika karne ya 19 huko ulaya wakati wafanyakazi kwenye viwanda vya nguo na vingine walipoamua kudai maslahi na mazingira bora ya kufanyia kazi. Maandhimisho hayo mwaka huu yanaongozwa na kaulimbiu isemayo ‘mshahara duni, kubwa kubwa na mfumuko wa bei ni pigo kwa wafanyakazi’.
 =30=  



SERIKALI KUTATUA KERO ZA WAFANYAKAZI 

MUFINDI

Serikali itaendelea kutatua kero za wafanyakazi ili kuwawezesha wanyakazi kufanya kazi katika mazingira bora na rafiki ili wazidishe ufanisi katika utendaji kazi wao.

Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma wakati akiongea na wafanyakazi wa Mkoa wa Iringa katika maadhimisho ya siku ya wafanyakazi duniani yaliyofanyika kimkoa mjini Mafinga wilayani Mufindi.

Dkt. Ishengoma amesema kuwa hapo awali zilikuwepo kero nyingi zilizokuwa zikiwakabili wafanyakazi, nakuzitaja kero hizo kuwa ni ucheleweshaji wa malipo kwa wastaafu, ucheleweshaji wa mishahara, na kero ya kutokupata mikopo katika benki. Amesema “hali hii sasa imerekebishwa na wafanyakazi ni mashahidi wa haya ninayoyazungumza, ingawa maboresho haya hayajafikia kiwango cha asilimia mia moja”. Amesema “kero inayoendelea hivi sasa ni suala la mishahara duni iliyo na kodi kubwa ambayo haiendani na hali ngumu kiuchumi inayoikabili nchi yetu.  Serikali inalitambua hilo na inaendelea kulifanyia kazi ili kuipatia ufumbuzi wa kudumu”.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa lazima wafanyakazi watambue nafasi yao katika jamii na kuwataka kufanya kazi kuwa juhudi, nidhamu na maarifa na kujituma kazini pasipo kufuatwafuatwa. Amesema kufanya hivyo kutawafanya wafanyakazi kuheshimika katika jamii. Amewataka waajiri kuendelea kutoa vitendea kazi bora na kutoa kujali usalama wa wafanyakazi wote ili kuboresha utendaji kazi wao.

Aidha, Dkt. Ishengoma amevitaka vyama vya wafanyakazi kuwajibika kuwaelimisha wanachama wao ambao ni watumishi wa Serikali, Taasisi, Mashirika mbalimbali, Watumishi wa hotelini na Majumbani pamoja na Wafanyakazi wengine juu ya kuheshimu nafasi waliyopewa katika jamii na kuelewa msingi wa utumishi bora kwa Umma.

Akiongelea mchakato wa uundwaji wa Katiba Mpya, Mkuu wa Mkoa amewataka wafanyakazi wote kushiriki katika kuhamasisha na kuwaeleza wananchi ili washiriki katika mchakato huo kwa kutoa elimu. Amesema “napenda kutoa wito kwa wananchi wote kuwa huru kutoa maoni yenu kwa Tume itakapopita na kukusanya maoni yenu”.

Chimbuko la maadhimisho ya siku ya wafanyakazi duniali lilianza karne ya 19 huko ulaya na mwaka huu Kauli Mbiu ya Maadhimisho haya ni ‘maisha duni, kodi kubwa na mfumuko wa bei ni pigo kwa wafanyakazi’.

=30=





WAANDISHI HABARI HAMASISHENI SENSA

Mkuu wa Mkao wa Iringa amewataka waandishi wa habari, viongozi wa dini na wazee mashuhuri Mkoani Iringa kuhamasisha wananchi juu ya uelewa wa Sensa ya watu na Makazi ili waweze kujitokeza na kuhesabiwa hapo Agosti 26, 2012.

Wito huo ameuto Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma katika taarifa yake aliyoitoa kwa waandishi wa habari, viongozi wa dini, wazee mashuhuri na vyombo vya ulinzi na usalama kuhusu uhamasishaji wa wananchi kushiriki katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi leo alipokutana nao katika ukumbi wa mikutano wa ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa.

Dkt. Christine amesema kuwa kutokana na umuhimu wa Sensa ya Watu na Makazi nchini, nafasi za makundi mbalimbali ni muhimu sana katika kusaidia kutoa elimu na hamasa, amesema “hamna budi kufahamu kuwa takwimu za Sensa ya Watu na Makazi ndizo zitakazoiwezesha Serikali kutambua hali halisi na mahitaji halisi ya huduma zilipo katika maeneo yenu hivyo kuingizwa katika mipango ya maendeleo ya taifa”.

Amesema kutokana na msingi huo makundi hayo aliyokutana nayo yanapaswa kuhamasisha wananchi ili waweze kuhesabiwa na kusisitiza kuwa kuhesabiwa huko iwe ni mara moja tu kuwezesha takwimu zitakazokusanywa ziwe sahihi na za uhakika. Amesema kuwa iwapo takwimu zote zitakazokusanywa zitakuwa sahihi, huo ndio utakuwa utimilifu wa takwimu za Sensa kitaifa.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa mambo muhimu ya kuzingatia wakati ya kuhamasisha wananchi ni pamoja na tarehe ya Sensa, umuhimu wa Sensa na yatakayojiti wakati wa zoezi la kuhesabu watu.
Akiwatoa hofu wananchi kuhusu mawazo potofu dhidi ya zoezi la Sensa, Mratibu wa Sensa Mkoa wa Iringa, Fabian Fundi amesema kuwa zoezi la Sensa ya Watu na Makazi halihusiani kabisa na hofu walizonazo wananchi. Amesema “ni muhimu sana kuwatoa hofu wananchi kwa kuwaelimisha kuwa zoezi la Sensa halihusiani kabisa na hofu au imani walizonazo”.

Fundi, amesisitiza kuwa wananchi wawe huru kutoa taarifa watakazoulizwa katika dodoso na kuwahakiihsia kuwa taarifa hizo zitatumika kwa mambo ya kitakwimu pekee na kwa usiri mkubwa.

Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Gertrude Mpaka amesema amewataka wananchi kuwatoa watoto wote na watu wenye ulemavu ili waweze kuhesabiwa na kuiwezesha Serikali kuangalia njia bora ya kuwahudumia vizuri zaidi. Aidha, amekemea tabia ya baadhi ya wanajamii kuwaficha watoto wenye ulemavu katika shughuli mbalimbali kutokana na ulemavu walionao.
=30=

Tuesday, April 17, 2012

SHERIA YA BIMA YA AFYA KUBORESHA HUDUMA ZA AFYA NCHINI

Serikali ya Tanzania iliamua kupitisha Sheria ya kuanzishwa kwa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na Mfuko wa Afya ya Jamii kwa lengo la kurahisisha upatikanaji wa huduma za afya kwa kila mtu kwa kuchangia kidogo ili kumuwezesha mwanachi kutibiwa hata kama hana fedha pindi anapougua.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa mkoa wa Iringa, Dr. Christine Ishengoma, katika hotuba yake ya ufunguzi wa kongamano la wadau wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya wa Mikoa ya Iringa na Njombe uliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Highland, Manispaa ya Iringa.

Dr. Ishengoma amesema “lengo kuu wa kupitishwa kwa Sheria hii ilikuwa ni kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa kila mtu kwa kuchangia kiwango kidogo kabla ya kuugua, ili anapougua aweze kutibiwa hata kama hatakuwa na fedha za kulipia wakati huo”. Amesema kutokana na gharama za matibabu kuwa juu jambo linalomuwia ugumu mwananchi wa kumudu, ndio msingi ulioifanya Serikali kuanzisha utaratibu wa mwananchi kulipia gharama za matibabu kabla ya kuugua kwa utaratibu wa Bima. Amesema ili utaratibu huu uwe mahususi Serikali ilitunga Sheria inayoanzisha Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na Mfuko wa Afya ya Jamii.

Mkuu wa Mkoa amesema kuwa afya bora ni jambo muhimu sana kwa wananchi na ndio chachu ya wananchi kujiletea maendeleo kutokana na uzalishaji sababu kama wananchi hawatakuwa na afya nzuri na imara uzalishaji utashuka na jamii kuendelea kuwa masikini. Amesema kuwa familia inayosumbuliwa na maradhi muda mwingi haiwezi kuzalisha mali.Amesema suluhisho lake ni familia kuwa na uhakika wa matibabu pindi wakiugua, ni vema kuhimiza wananchi kujiunga na Mifuko ya afya ya Jamii katika Halmashauri.

Dr. Ishengoma alionesha kusikitishwa sana na takwimu zinazoonesha kuwa kati ya mwezi Desemba, 2009 na Desemba, 2011 jumla ya shilingi bilioni 3.5 zililipwa na serikali kwa Halmashauri nchini kama tele kwa tele. Kati ya fedha hizo mikoa ya Iringa na Njombe haijaambulia chochote.

Nae Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Aseri Msangi amewataka viongozi wa bima ya afya katika ngazi za mikoa kuwasilisha taarifa zao katika ofisi ya waku wa wilaya na mikoa ili ziwawezeshe kupanga ratiba za ufuatiliaji na kuhamasisha uhamasishaji kwa wananchi ili mfuko huo wa afya ya jamii iweze kuwa na manufaa na endelevu. Aesema pia changamoto ya mawasiliano na uelewa mdogo pia inahitaji kuangaliwa kwa jicho la karibu na wadau wa bima ya afya kwa lengo la kupanua uelewa wao na wananchi kwa ujumla.

Kaimu Mkurugenziwa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Immaculate Senje, amesema kuwa ili mfuko wa Afya ya Jamii uweze kuwanufaisha wananchi wengi, suala la uhamasishaji jamii linahitaji kupatiwa uzito unaostahili. Amesema kuwa wananchi wapo tayari hasa pale wanapohamasishwa na viongozi na kupatiwa taarifa sahihi hasa manufaa yanayotokana na kujiunga na mfuko huo.


Thursday, April 12, 2012

MALEZI YA WATOTO YAHIMIZWA IRINGA

Na. Dennis Gondwe, IRINGA
Serikali Mkoani Iringa imesema kuwa itaendelea kushirikiana na taasisi binafsi katika kuhakikisha kuwa malezi mazuri yanatolewa kwa watoto na kuwasaidia watoto walio katika mazingira hatarishi ili nao waweze kufurahia matunda ya uhuru kama watoto wengine kwa kuwa na maadili mema.

Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma katika hotuba yake iliyosomwa na Mwl. Joseph Mnyikambi, Kaimu Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Huduma za Jamii iliyemuwakilisha Mkuu wa Mkoa katika hafla ya ugawaji wa zawadi kwa watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi wa Manispaa ya Iringa chini ya shirika lisilo la kiserikali la Operation Christmas Child lenye makao yake Makuu nchini Marekani iliyofanyika katika ukumbi wa IDYDC Manispaa ya Iringa.

Mwl. Mnyikambi amesema kuwa “nimefahamishwa kuwa taasisi hii ya OCC pia inatoa mafunzo yanayolenga maadili. Nawapongeza sana kwa sababu jamii yenye maadili mema ndiyo jamii inayofanikiwa katika maisha”.

Amesema kuwa “ili jamii ifanikiwe katika maisha basi msingi wake lazima jamii hiyo iwekeze katika malezi na makuzi ya watoto katika maadili”. Ametoa wito kwa jamii kulipa kipaumbele suala la maadili kwa watoto na vijana ili kujenga taifa imara na makini.

Amesema kuwa suala la maadili ni suala la upendo katika jamii na kusisitiza kuwa kinyume chake ni mmomonyoko wa maadili katika taifa zima. Amesema kuwa jamii kwa sasa inashuhudia watoto wakitumia dawa za kulevya, ulevi wa kupindukia, lugha za matusi na watoto wa kiume kusuka nywele jambo linalowafananisha na watoto wa kike na kufanya vitendo visivyo vya kibinadamu kama ubakaji wa watoto wadogo.

Katika risala yao iliyosomwa na Mratibu wa Operation Christmas Child Askofu Dk. Boaz Sollo ameishukuru serikali kwa kusamehe kodi na kuiomba kupitia mamlaka ya bandari kuweka mfumo rahisi zaidi wa kutoa vitu bandarini ili kupunguza au kuondoa gharama zinazotokana na uhifadhi wa mizigo hiyo bandarini.

Aidha, ameishauri serikali kuwa macho zaidi na yeyote anayejaribu kuhatarisha amani kwa kutumia dini au siasa ili nchi iiendelee kuwa na amani na utulivu. Amesema kuwa mwaka huu kwa Mkoa wa Iringa umepokea jumla ya mabox 3500 ya zawadi kwa ajili ya watoto 3500.

=30=



Friday, March 16, 2012

TANZANIA YABORESHA HUDUMA ZA MAJI

Na.
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekuwa ikiboresha upatikanaji wa huduma za kiuchumi na kijamii ukiwemo mpango wa kuboresha usimamizi na rasilimali za maji na kuboresha upatikanaji wa huduma za maji safi, usafi wa mazingira na maji kwa ajili ya umwagiliaji.

Akiongea wakati wa uzinduzi wa maadhimisho ya wiki ya maji kitaifa mkoani Iringa, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma, aliyemuwakilisha Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, George Mkuchika amesema kuwa “Serikali kupitia Dira ya Maendeleo ya Taifa, Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini -MKUKUTA, na mabadiliko mbalimbali ya kisera na kimfumo, imekuwa ikitekeleza mipango mbalimbali ya kuboresha upatikanaji wa huduma za kiuchumi na kijamii ikiwemo mpango wa kuboresha usimamizi na rasilimali za maji, kuboresha upatikanaji wa huduma za majisafi, usafi wa mazingira na maji kwa ajili ya umwagiliaji”.

Amesema kuwa kwa sasa Serikaili inatekeleza mpango wa pamoja wa matumizi ya rasilimali za maji kupitia ofisi zote tisa za mabonde nchini. Amesema pindi mpango huo utakapokamilika utaainisha njia za matumizi bora ya rasilimali maji.

Amesema “katika kuhakikisha rasilimali ya maji inatumika kwa manufaa ya taifa na usalama wa chakula nchini unakuwepo, ninawaomba viongozi wenzangu, vyombo vinavyosimamia rasilimali maji kama vile Mamlaka za Maji, Ofisi za Maji za Mabonde, Vyombo vya Watumiaji Maji na wananchi kwa ujumla kujiandaa kuzikabili changamoto na vihatarishi nilivyotaja”.

Ameitaka jamii kushirikiana katika kuhifadhi, kutunza na kuendeleza mfumo mzima wa maji kuanzia kwenye vyanzo, uzalishaji na ugawaji kwa kuzingatia ongezeko la matumizi ya maji.

Mkoa wa Iringa ni mwenyeji wa maadhimisho ya 24 ya wiki ya maji kitaifa yanayoongozwa na kauli mbiu isemayo ‘maji kwa usalama wa chakula’, shughuli mbalimbali za sekta ya maji pamoja na maonesho zitafanyika katika uwanja wa Samora na maeneo mengine.
=30=

MAAFISA KILIMO WATAKIWA KUFANYA MABADILIKO

Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika amewataka maafisa kilimo na wadau wa sekta hiyo kufanya mabadiliko makubwa katika kukuza sekta hiyo ili iwe ya kisasa na kuifanya iwanufaishe wananchi wengi zaidi.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Prof. Jumanne Maghembe, wakati akifungua mkutano wa maafisa kilimo wa Tanzania bara, uliofanyika katika hoteli ya royal village, katika Manispaa ya Dodoma.

Prof. Maghembe amesema kuwa asilimia 77.5 ya wananchi wanaokadiriwa kufika mil. 40 wanategemea sekta ya kilimo katika kuendeleza maisha yao na kati yao asilimia 22.5 ndiyo wanaofanya kazi katika sekta hiyo.

Amesema pamoja na ukubwa wa asilimia ya wananchi wanaotegemea sekta hiyo  bado kilimo kinachangia asilimia 34 tu ya fedha za kigeni nchini. Katika mchango wa kilimo katika pato la taifa, kinachangia asilimia 24 pekee. Amesema “bado kazi inatakiwa kufanywa na sisi tuliomo humu ndani, tumeandaliwa vizuri kitaaluma ili tuweze kutekeleza hili, kushindwa tunaliangusha taifa”.    

Prof. Maghembe amesema kuwa kilimo nchini kinakua kwa asilimia 4.2 tofauti na lengo la kitaifa la kilimo kukua kwa angalau asilimia 6 kwa mwaka.

Pamoja na kuhimiza kilimo cha umwagiliaji, Waziri wa kilimo, Chakula na Ushirika amesema “suala si kuongeza maeneo ya kulima, bali ni kuongeza uzalishaji katika maeneo tunayolima”.

Akiongelea vikwazo vinavyoikabili sekta ya kilimo, amesema kuwa masoko yasiyo ya uhakika dunia na kuwataka wadau hao kujipanga katika kukuza kilimo ili kiweze kuzinufaisha nchi zenye upungufu wa chakula na kuzifanya zisifikirie kununua chakula sehemu nyingine zaidi ya Tanzania.

Akichangia katika mkutano huo huku akisikilizwa kwa umakini mkubwa na mkutano huo, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma amesema kuwa nchi haiwezi kuwa na mafanikio katika sekta ya kilimo bila kuendeleza kilimo cha umwagiliaji. Amesema ni vema juhudi zikawekwa katika kufufua kilimo cha umwagiliani pamoja na kuimarisha skimu za umwagiliaji ili kilimo kiweze kushamiri.

Akichangia katika upatikanaji wa soko, Dk. Ishengoma amesema kuwa soko ni changamoto kuwa kwa kufanikisha shughuli za kilimo. Amesema ukitangaza uhakika wa soko la mazao mapema wakulima watalima kwa nguvu kwa sababu watakuwa na uhakika na soko. Akitolea mfano katika mkoa wake wa Iringa, amesema kuwa mkoa huo umehimiza kilimo cha zao la mtama kwa wingi ili kukabiliana na changamoto ya upungufu wa chakula, muitikio umekuwa mzuri baada ya kuwa na uhakika wa soko.

Changamoto nyingine ameitaja kuwa ni upungufu wa fedha za ufuatiliaji, hatua inayowakwamisha wataalamu wa kilimo katika kutekeleza majukumu yao katika sekta ya kilimo.
=30=

Thursday, March 15, 2012

WIKI YA MAJI IRINGA


Mkoa wa Iringa umepewa heshima ya kuwa mwenyeji wa maadhimisho  ya 24 ya wiki ya Maji kitaifa yatakayofanyika kuanzia tarehe 16 hadi 22 Machi, 2012.
Katika taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma (Mb.) leo, amesema kuwa uzinduzi na kilele cha maadhimisho vitafanyika katika uwanja wa Samora uliopo katika Manispaa ya Iringa.
Amesema kuwa maadhimisho yaho yanaongozwa na kaulimbiu isemayo ‘maji kwa usalama wa chakula’ yanalenga kuwaelimisha wananchi kuhusu Sera ya Maji na majukumu ya wananchi katika kuitekeleza sera hiyo. Amesema madhumuni mengine ni kutathmini maendeleo ya utekelezaji waprogramu ya maji, hali ya huduma ya maji na usafi wa mazingira na kuweka mikakati ya kuboresha utoaji wa huduma na uhifadhi wa rasilimali za maji.
Dk. Christine amesema kuwa maadhimisho hayo pia yanalenga kutoa ujumbe kwa wadau kuhusu kaulimbiu ya wiki ya maji na siku ya maji Duniani na kuhamasisha wananchi na wadau wengine kushiriki katika kupanga, ujenzi, uendeshaji na matengenezo ya miradi ya maji na usafi wa mazingira. Vilevile, maadhimisho ya wiki ya maji yanalenga kujenga na kuimarisha mshikamano miongoni mwa wadau wa sekta hiyo.
Akiongelea maandalizi na matukio ya maadhimisho ya hayo, Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa maandalizi hayo yanaendelea vizuri na uzinduzi na kilele cha maadhimisho vitahusisha viongozi wa kitaifa. Amesema kuwa matukio ya mwaka 2012 yanalenga kuwashirikisha wadau na wananchi wote kwa pamoja kupanga, kujenga, kuendesha na kufanya matengeneza miradi ya maji na kuimarisha usafi wa mazingira sambamba na kutunza vyanzo vya maji.
Dk. Christine amezitaja shughuli zitakazofanyika katika maadhimisho hayo kuwa ni uzinduzi wa miradi ya maji ambayo ujenzi wake umekamilika. Amesema kuwa miradi mingi imetekelezwa kupitia programu ya maendeleo ya sekta ya maji na wadau mbalimbali.
Kuhusu unufaishaji wa miradi hiyo itakayozinguliwa, Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa miradi hiyo itawanufaisha wananchi wapao 184,900.
Mkuu wa Mkoa amesema kuwa maadhimisho hayo kitaifa yatagharamiwa na Wizara ya Maji, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mamlaka za Majisafi na majitaka nchini, Halmashauri, Taasisi na Mashirika ya kiserikali na yasiyo ya kiserikali na wamiaji maji. Vilevile, amewashukuru wadau wote kwa utayari wao wa kuchangia ili kufanikisha maadhimisho hayo.
=30=


IRINGA MWENYEJI WIKI YA MAJI KITAIFA



Mkoa wa Iringa umepewa heshima ya kuwa mwenyeji wa maadhimisho ya 24 ya wiki ya Maji kitaifa ambapo shughuli na maonesho ya vifaa na teknolojia usambazaji maji na usafi wa mazingima vitafanyika ili kutoa ujumbe uliokusudiwa kwa wananchi.
 
Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari ofisini kwake, Mkuu wa Mkoa wa Iringa ambaye ndiye mwenyeji wa maadhimisho hayo Dk. Christine Ishengoma amesema kuwa maadhimisho hayo yatafanyika katika Mkoa wa Iringa kuanzia tarehe 16-22 Machi, 2012. amesema “kilele cha maadhimisho kitakuwa tarehe 22 Machi ambayo  siku hiyo inafahamika Kimataifa kuwa ni Siku ya Maji Duniani kwa mujibu wa Azimio Na. 193/47 la Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa”. Amesema kuwa uzinduzi na kilele cha wiki ya maadhimisho hayo kitakuwa katika uwanja wa Samora, Manispaa ya Iringa.
 
Amesema miongoni mwa shughuli zitakazofanyika katika maadhimisho hayo ni pamoja na kufanya usafi wa mazingira katika vyanzo vya maji, matanki na visima vya maji katika miji na vijiji mbalimbali mkoani Iringa.
 
Amesema kuwa shughuli nyingine ni maonesho ya vifaa na teknolojia za usambazaji wa maji na usafi wa mazingira vitafanyika katika uwanja wa Samora uliopo katika Manispaa ya Iringa na kusisitiza kuwa maonesho yatafanyika muda wote wa maadhimishoyo ya wiki ya Maji.
 
Dk. Ishengoma amesema kuwa maadhimisho ya wiki ya maji mwaka 2012 yanaongozwa na kaulimbiu isemayo “maji na usalama wa chakula”. Kuhusu madhumuni ya maadhimisho hayo, amesema kuwa yanalenga kutathmini maendeleo ya utekelezaji wa programu ya maji, hali ya huduma ya maji na usafi wa mazingira na kuweka mikakati ya kuboresha utoaji wa huduma na uhifadhi wa rasilimali za maji. Maadhimisho hayo pia yanalenga kutoa ujumbe kwa wananchi juu ya kaulimbiu ya wiki ya maji na siku ya maji duniani pamoja na kuimarisha mshikamano baina ya wadau wa sekta ya maji.
 
Maadhimisho haya pia yanalenga kuhamasisha wananchi kushiriki katika kupanga, ujenzi na uendeshaji na matengenezo ya miradi ya maji na usafi wa mazingira na kutoa elimu juu ya sera ya taifa ya maji na utekelezaji wake.
 
Kuhusu maandalizi ya wiki ya maji, Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa maandalizi yake yanaendelea vizuri na uzinduzi na kilele cha maadhimisho hayo vitawahususha viongozi wa kitaifa. Amesema kuwa shughuli mbalimbali zitafanyika katika maadhimisho hayo zikiwa ni uzinduzi wa miradi ya maji ambayo ujenzi wake umekamilika. Kuhusu ugharimiaji wa miradi hiyo, Dk. Ishengoma amesema kuwa miradi mingi imetekelezwa kupitia programu ya maendeleo ya sekta ya maji na wadau mbalimbali. Amesema jumla ya wananchi 184,900 wananufaika na miradi itakayozinduliwa.
 
Ikumbukwe kuwa kila mwaka kuanzia mwaka 1988, Tanzania imekuwa ikiadhimisha Wiki ya Maji kuazia tarehe 16-22  Machi kwa kuwahusisha wananchi na wadau wote wa maji. 

Monday, March 5, 2012

VP AWATAKA WANAWAKE KUHUDHURIA KLINIKI

Makete
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Mohamed Gharib Bilal amewataka wanawake Mkoani Iringa kuhakikisha wanahudhuria kliniki tokea hatua za awali za ujauzito ili waweze kutapa huduma za kitaalamu mapema.

Kauli hiyo ameitoa katika eneo la Mfumbi wilayani Makete alipokuwa akisalimia wananchi wa wilaya ya hiyo baada ya kuweka jiwe la msingi soko lililojengwa kwa nguvu za wananchi na kupokea taarifa ya Mkoa na wilaya ya Makete alipowasili mkoani Iringa kuanza ziara yake ya siku tatu mkoani hapa akitokea mkoani Mbeya.

Dk. Bilal amewata mkoani hapa kuhudhuria kliniki ili kunufaika na huduma za afya na ushauri kwa wajawazito kutokana na serikali kuwekeza sana katika afya ya mama na mtoto.

Akiongelea maambukizi ya Ukimwi, Makamu wa Rais amesema kuwa taifa bado linakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo idadi ya maambukizi ya Ukimwi na kuitaka jamii kuwa makini zaidi na kujilinda. Vilevile, ameitaka jamii kuendelea kushirikiana na juhudi za serikali kupambana na maambukizi ili kupunguza idadi ya vifo nchini.

Katika taarifa ya maendeleo ya mkoa wa Iringa, iliyowasilishwa kwa Makamu wa Rais na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma, amesema kuwa mkoa umeongeza vituo vya kutolea huduma za Afya hadi kufikia 420  kwa lengo la kutoa huduma bora za afya kwa kuzingatia mahitaji ya makundi maalumuhasa watoto wachanga na walio na umri chini ya miaka mitano, wazee na wanawake walio katika uzazi.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa katika kutekeleza sera ya zahanati kwa kila kijiji, mkoa umefikia asilimia asilimia 57 ya vijiji vyote kuwa na zahanati wakati asilimia 23 ya kata zote zina vituo vya afya.

Akiongelea huduma za mama wajawazito na watoto, Dk. Ishengoma amesema kuwa katika mwaka 2011 akina mama waliojifungulia kliniki walikuwa ni 54,356 sawa na asilimia 57.3 ya akina mama wajawazito waliotarajiwa kuhudhuria huduma za kliniki.

Amesema kuwa kiwango cha akina mama wajawazito waliojifungulia katika vituo vya tiba imefikia asilimia 76.2.

Amesema kuwa vifo vya wazazi vimepungua kutoka 162/100,000 mwaka 2010 hadi kufikia 138/100,000. Aidha, vifo vya watoto vimepungua kutoka 21/1,000 hadi 17/1,000.

Makamu wa Rais yupo katika ziara ya kikazi ya siku tatu mkoani Iringa.
 =30=




 MAKETE WATAKIWA KUKITUMIA CHUO CHA VETA
Makete
Wananchi wa Wilaya ya Makete wametakiwa kuonesha kuwa wapo tayari kukitumia chuo cha ufundi stadi VETA kwa kujipanga vizuri kukitumia na kukiendeleza chuo hicho ili kiweze kuwanufaisha wakazi wa wilaya ya Makete na taifa kwa ujumla.

Rai hiyo imetolewa na Makamu wa Rais, Dk. Mohamed Gharib Bilal wakati akizungumza na wakazi wa wilaya ya Makete baada ya kuweka jiwe la msingi ujenzi wa chuo cha ufundi stadi VETA wilayani hapa.

Dk. Bilal amesema kuwa “wilaya ya Makete tumepata fursa kubwa kuwa na VETA Makete” na kuutaka uongozi wa wilaya hiyo kujipanga vizuri kuonesha kuwa wao ni namba moja kwa kujenga uhusiano mzuri kati ya VETA Makete na mamlaka ya ufundi stadi nchini.

Amesema kuwa siku zote VETA lazima iwe karibu na jamii inayoihudumia kwa kutokuweka mwanya kati yake ili jamii inufaike na VETA na kinyume chake.
Makamu wa Rais ameutaka uongozi wa VETA wilaya ya Iringa kutafakari kwa kina kile kinachoitajika katika jamii hasa wakati uliopo sasa na kutoka na masuluhisho ya matatizo yaliyopo katika jamii.

Amesema kuwa ili wananchi wapige hatua hawana budi kukifahamu chuo cha VETA na matarajio yake katika kuihudumia jamii ili kuisaidia kupiga hatua ya kimaendeleo.

Aidha, amekitaka chuo hicho kutoa wanafunzi waliopikika na kuiva ili kukabiliana na ushindani uliopo katika soko na kuleta picha nzuri katika jamii. Amesema wakati mambo mengi yanakua kwa haraka, elimu ya ufundi stadi inatakiwa kupanuliwa zaidi kwa kuhusisha teknolojia ya habari kuwafikia watu wengine wali mbali zaidi na kuwafanya wanufaike na huduma hizo.

Katika taarifa ya Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugu amesema kuwa hivi karibuni nchi za afrika Masharki zitafungua milango yake itakayomtaka mtu mmoja kwenda kusaka ajira katika nchi nyingine. Amesema kwa muktadha huo “hatuna budi kuwaandaa vijana wetu katika elimu ya ufundi stadi ili wasiwe watazamaji”. Amesema kuwa serikali inaendelea na upanuaji wa mafunzo stadi ili kuwawezesha vijana wengi kujiunga na mafunzo hayo. Ameongeza kuwa serikali itaendelea kuongeza kasi ya ujenzi wa vyuo vya ufundi na kuboresha utoaji wa elimu bora ya mafunzo stadi nchini.

Chuo cha ufundi stadi VETA wilaya ya Makete ndicho chuo cha kwanza kwa mujibu wa sera ya chama tawala ya kujenga chuo cha VETA kila wilaya nchini na kinatajia kuanza mwezi Julai 2012 kwa kuanza na wanafunzi 160 katika fani za ujenzi, uashi, uselemala, ufundi wa magari.

=30=   


KILIMO CHA MTAMA CHAHIMIZWA IRINGA
 Makete
Mkoa wa Iringa unahimiza kilimo cha mtama, mihogo na mazao mengine yanayovumilia ukame ukiwa ni mkakati wa kukabiliana na hali ya ukame wa mara kwa mara unaosababisha upungufu wa chakula kwa baadhi ya maeneo mkoani hapa.

Katika taarifa ya maendeleo ya mkoa wa Iringa iliyowasilishwa kwa Makamu wa Rais, na Mkuu wa Mkoa wa Iringa Dk. Christine Ishengoma amesema kuwa ushauri wa kilimo cha mazao yanayovumilia ukame kama mtama, mhogo na mazao mengine umetolewa kwa Halmashauri zenye maeneo ya ukame ili kukabiliana na hali ya ukame wa mara kwa mara.

Amesema viongozi na wataalamu wa wilaya ya Iringa, Kilolo pamoja na Mkoa walitembelea kilimo cha mtama wilaya ya mpwapwa mwezi Mei, 2011 ili kujifunza uzalishaji wa zao la mtama ili waweze kuhimiza kilimo hicho maeneo yote yanayokabiliwa na ukame katika wilaya hizo.

Katika kuhakikisha hamasa inakuwepo katika kilimo hicho Mkuu wa Mkoa wa Iringa alifanya ziara katika wilaya hizo kuhimiza kilimo cha mazao yanayostahimili ukame ili kuzifanya kaya zinazokabiliwa na upungufu wa chakula kuwa na uhakika wa chakula.

Amesema kuwa kila mkulima amehimizwa kulima ekari mbili za mtama kwa lengo la kuwa na uhakika wa chakula. Amesema kuwa kila shule katika maeneo hayo imetakiwa kulima ekari mbili kwa ajili ya chakula cha wanafunzi wakati wa mchana.

Amesema kuwa viongozi wote kuanzia ngazi ya wilaya hadi kijiji nao wamelima ekari mbili za mtama kila mmoja na muitikio wa agizo hilo umepokelewa vizuri.  

Akiongelea sekta ya afya, Mkuu wa Mkoa amesema kuwa hadi kufikia mwaka 2011 akina mama waliohudhuria kliniki ni 54,356 sawa na asilimia 57.3 ya akina mama wajawazito waliotarajiwa kuhudhuria huduma za kliniki. Aidha, amesema kuwa kiwango cha akina mama wajawazito waliojifungulia katika vituo vya tiba imefikia asilimia 76.2.

Amesema kuwa vifo vya wazazi vimepungua kutoka 162/100,000 katika mwaka 2010 hadi kufikia 138/100,000, wakati vifo vya watoto vimepungua kutoka 21/1,000 hadi kufikia 17/1,000.

Akiongelea hali ya maambukizi ya UKIMWI, Dk. Ishengoma amesema kuwa maambukizi yamefikia asilimia 15.7 na mkoa katika kukabiliana na hali hiyo mkoa uliandaa mpango wa miaka minne wa kupambana na maambukizi ya UKIMWI unaoendelea kutekelezwa. Amesema mpango huo ulioandaliwa na wadau wa sekta binafsi na umma ni wa kuanzia Oktoba 2008 hadi Septemba, 2012. 

Katika salamu za Makamu wa Rais, Dk. Mohamed Gharib Bilal kwa wananchi wa Mfumbi wilaya ya Makete amesema kuwa taifa bado linakabiliwa na changamoto mbalimbali pamoja na idadi ya maambukizi ya UKIMWI na kuwataka wananchi kuwa makini zaidi na kujilinda. Amewataka kuendelea kushirikiana na serikali katika kuhubiri mapambano hayo ili kupunguza maambukizi.

Dk. Bilal pia amewataka akina mama wajawazito kuhudhuria kliniki mara kwa mara pindi wanapojigundua kuwa ni wajawazito ili waweze kunufaika na huduma hizo zinazotolewa kwa ajili yao.

Makamu wa Rais, anafanya ziara ya kikazi ya siku tatu mkoani Iringa katika wilaya za Makete, Njombe, Mufindi na Iringa na akiwa wilayani makete ameweka jiwe la msingi mradi wa soko lililojengwa kwa nguvu za wananchi katika kijiji cha Mfumbi, kuzindua nyumba ya walimu  katika sekondari ya Kitulo na kuweka jiwe la msingi chuo cha VETA.
=30=

Wednesday, February 15, 2012

Mgodi wa Tarajali kuanza Ruvuma

Na. Revocatus Kassimba, Ruvuma
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Mohamed Ghalib Bilal amewahakikishia wakazi wa Mkoa wa Ruvuma na Tanzania kwa ujumla kuwa  mradi wa mgodi tarajali wa Urani wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma utatekelezwa kwani una umuhimu na maslahi kitaifa.

 Makamu Rais Dk. Mohamed Ghalib Bilal akihutubia mamia ya wananchi wa kijiji cha Likuyu Sekamaganga wilaya ya Namtumbo wakati alipofanya ziara katika mradi wa urani

Dk. Bilal amesema hayo wakati akiongea na wafanyakazi wa mgodi huo unaomilikiwa na kampuni ya Mantra Tanzania kuwa Serikali inafuatilia kwa makini kuona madini hayo muhimu yanalifaidisha Taifa.

Aliongeza kuwa anao uhakika kuwa taratibu zote za hifadhi ya mazingira na usalama wa maisha ya wakazi wanaozunguka eneo hilo umetiliwa mkazo na kampuni kwa kushirikiana na taasisi ya nishati ya atomiki nchini.

Aidha, kwa upande wake Mkurugenzi wa Mantra Tanzania, Asa Mwaipopo ameiomba Serikali kuharakisha taratibu za kisheria ili mgodi uweze kuanza hapo mwaka ujao kwa ujenzi na ifikiapo 2014 uzalishaji uanzae ili ajira zipatazo 1600 wakati wa ujenzi wa mgodi na nyingine 400 wakati wa uzalishaji ziweze kupatikana kwa watanzania na kusaidia kukuza uchumi.

 
Makamu wa Rais akipokewa na viongozi wa kampuni ya Mantra wakati alipowasili katika eneo litakalojengwa mgodi wa Uranium wilaya ya Namtumbo


Monday, February 6, 2012

Ruvuma na Cuba


Na. Revocatus Kassimba, Songea
Serikali mkoani Ruvuma imeihakikishia nchi ya Cuba kuendeleza ushirikiano  ili kuboresha mahusiano mema yaliyojengeka kwa miongo zaidi ya minne hususan katika kuendeleza huduma za afya nchini.
Kauli hiyo imetolewa leo mjini Songea na Kaimu Katibu Tawala  Mkoa wa Ruvuma  Dkt Anselm Tarimo alipokuwa akiongea na Balozi wa Cuba nchini Ernesto Gomez Diaz alipofanya mazungumzo na uongozi wa Sekretariati ya Mkoa wa Ruvuma.
Dkt Tarimo alielezea Uhusiano wa kiurafiki uliopo na nchi ya Cuba kuwa umesaidia sana katika jitihada za serikali ya Tanzania kuwapatia wananchi wake Huduma bora  na za uhakika za afya.
Alisema kwa kipindi kirefu nchi ya Cuba imekuwa ikisaidia Tanzania kwa kuipatia wataalam wa afya hususan madaktari wanaofanya kazi katika hospitali mbalimbali nchini ambapo katika mkoa wa Ruvuma wapo madaktari wawili kutoka nchini Cuba.
“Tunashukuru kwa ushirikiano tulionao baina ya nchiz zetu mbili kwani kuanzia miaka ya 1980 mkoa wetu umekuwa ukipokea madaktari kutoka nchini Cuba ambao wanasaidia kutoa Huduma za tiba katika hospitali yetu ya Mkoa Songea” alisema Dkt Tarimo
Aliongeza kusema kwa sasa mahitaji ya madaktari ni makubwa kutokana na hospitali ya mkoa kupandishwa hadhi na kuwa ya rufaa hivyo ni vema Cuba ikaongeza wataalam zaidi
Naye Balozi wa Cuba nchini Ernesto Gomez Diaz alishukuru serikali ya Tanzania chini ya uongozi wa Rais Jakaya Kikwete kwa kuendeleza na kudumisha ushirikiano kati ya nchi zote mbili  toka enzi za waasisi  Mwalimu Julius Nyerere wa Tanzania na Fidel Castro wa Cuba
Balozi Diaz amesema Cuba ni nchi pekee iliyobaki inayofuata mfumo wa Ukoministi  Duniani wenye lengo la kuhakikisha maisha ya kijamaa ambapo rasilimali za umma zinatumika kwa wote
Aliongeza kusema kuwa katika nchi ya Cuba kutokana na sera ya Ukoministi serikali imefanikiwa kutoa Huduma za afya na Elimu bure kwa raia wake wote na kusema kuwa nchi yake itaendelea kutoa kipaumbele kwa watanzania kwenda kusoma udaktari nchini Cuba .
Balozi Diaz yupo mkoani Ruvuma kwa ziara ya kikazi ya siku mbili ambapo amepata fursa ya kutembelea na kukagua Hospitali ya mkoa ambapo nchi yake ina madaktari wawili wanaofanya kazi.
Ameshukuru uongozi wa serikali kwa kutoa ushirikiano kwa wataalam hao wa Cuba kwa kipindi chote wanachofanya kazi kwani wameendelea kufurahi uwepo wao hapa mkoani.

...RUVUMA WATAKIWA KULIMA MAHINDI KWA WINGI

Na. Revocatus Kassimba, SONGEA
Serikali imewataka wakulima  mkoani Ruvuma kulima kwa wingi mahindi katika msimu huu kwa kuzingatia kanuni bora za kilimo licha ya changamoto za soko lililowakabiri msimu wa kilimo uliopita.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Said Thabit Mwambungu wakati wa ziara yake katika vijiji vya Magagula, Lugagala na Muungano Zomba vilivyopo wilaya ya Songea .
Mwambungu aliwaeleza wananchi kuwa serikali inatambua kero ya ununuzi wa mahindi iliyotokea msimu wa 2011/2012 ambapo wakulima wengi walichelewa kupokea fedha zao kutoka Wakala wa Hifadhi za Chakula (NFRA).
Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu (mwenye kaunda suti nyeusi) akisikiliza maelezo ya kilimo kutoka kwa Mkuu wa wilaya ya Songea, Thomas Sabaya (kulia) wakati wa ziara ya kukagua usambazaji wa pembejeo za kilimo katika kijiji cha Lugagara wilaya ya Songea
Aliongeza kusema kuwa changamoto ya fedha za wakulima hazitajitokeza tena msimu ujao kwani tayari serikali imejiandaa kwa kutengwa fedha katika bajeti ili kuhakikisha mahindi yote yatanunuliwa kwa wakati.
“Limeni kuliko mwaka jana kwani serikali imejipanga kununua kwa wakati na kuhakikisha kuwa hakuna mkulima atakayecheleweshewa malipo na serikali” alisema Mwambungu na kuongeza kuwa hakuna mkulima sasa anayeidai serikali wote wamelipwa.
Mkuu wa mkoa Mwambungu alisisitiza kuwa serikali inafanya kila linalowezekana kuondoa kero ya kukopa mahindi ya wakulima hivyo ni vema wakulima wakaendelea kuunga mkono juhudi hizi za serikali kwa kuongeza uzalishaji.
Katika msimu 2011/2012 wa kilimo kwa mujibu wa taarifa za Wakala wa Hifadhi ya Chakula jumla ya tani 50,018 za mahindi zimenunuliwa kutoka kwa wakulima mkoani Ruvuma zenye thamani ya shilingi bilioni 17.5 ambapo kilo ilinunuliwa kwa shilingi 350.
Mkuu wa Mkoa alitumia fursa hiyo kuwapongeza wakulima wa vijiji hivyo alivyovitembelea kwa kutumia vema pembejeo za ruzuku kwa mfumo wa vocha kwani wameongeza uzalishaji wa mahindi na kuifanya wilaya ya Songea kuongoza katika kuzalisha mahindi mkoani.
Ziara ya Mkuu wa mkoa ilihusisha pia kukagua zoezi la ugawaji wa vocha za pembejeo ambapo kwa mujibu wa taarifa ya iliyotolewa na Mkuu wa wilaya ya Songea Thomas Sabaya alisema wilaya imepata mgao wa vocha 64,417 ambazo zimesambazwa kwa wakulima.

Wakulima wa kijiji cha Magagula Wilaya ya Songea wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu (hayupo pichani) jana alipofanya ziara ya kukagua shughuli za kilimo
Kuhusu mbolea ya kukuzia (UREA) mfuko unauzwa shilingi 72,000/= na mkulima anachangia shilingi 52,000/= huku serikali ikilipia zinazobaki na kwa mbegu bora mfuko unauzwa shilingi 40,000/= huku mkulima akichangia 20,000/= na serikali zinazobakia.
Kwa upande wake Afisa Mtendaji wa kijiji cha Lugagara Bi Taifa Mahundi katika risala yake alisema wakulima wana changamoto kubwa ya upungufu wa vocha za ruzuku hivyo akaiomba serikali kuongeza mgao kwa kijiji.
Mkuu wa mkoa akijibu hoja hiyo aliwafahamisha wananchi kuwa vocha zinazotolewa ni vigumu kufanana na idadi ya wakulima kwani hiyo ni ruzuku itolewayo na serikali kuwasaidia wakulima kujenga uwezo wa kujitegemea.
Katika msimu huu wa kilimo mkoa wa Ruvuma umepatiwa vocha za ruzuku ya pembejeo za kilimo 192,000 ambapo kwa mwaka uliopita ulipatiwa vocha 204,000 hivyo kuwa na upungufu wa vocha 12,000/=.
Mkoa wa Ruvuma ni kati ya mikoa sita maarufu kwa uzalishaji wa mahindi nchini ambapo mikoa mingine ni Iringa, Mbeya, Rukwa, Kigoma na Morogoro.
Sabaya alisema vocha hizo zinahusisha mbegu bora za mahindi, mbolea ya kupandia na mbolea ya kukuzia ambapo bei ya mfuko wa mbolea ya kupandia (DAP) inauzwa shilingi 80,000/=huku mkulima akichangia shilingi 52,000/=.

Sunday, January 22, 2012


Na. Revocatus Kassimba, Songea
Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu  amewaasa vijana waliohitimu mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa kuwa wazalendo na wenye kuipenda nchi yao ili waweze kuitumikia ili iweze kuwa na Maendeleo  endelevu
Ametoa wito huo leo wakati akifunga mafunzo awali ya kijeshi  yaliyojulikana kama Oparesheni  miaka 50 ya Uhuru yalitolewa katika kikosi cha jeshi 842 Mlale JKT  kilichopo wilaya ya Songea mkoa wa Ruvuma
Mwambungu amewapongeza Vijana hao kwa kuonyesha moyo wa uzalendo toka wajiunge na mafunzo hayo hapo mwaka jana julai ambapo wamejifunza mambo mengi yakiwepo stadi za kazi na mafunzo ya awali ya kijeshi
Aliongeza kusema mafunzo haya yatasaidia kujenga moyo wa kuipenda nchi hususan kipindi hiki ambapo maadili miongoni mwa Vijana yanaporomoka hivyo kwa kujiunga na jeshi la kujenga Taifa Vijana hupata Elimu na maarifa ya kujitegemea na hatimaye kuwa Vijana mahili katika Utendaji kazi
Alitumia pia fursa hiyo kuwapongeza Vijana wote walioshiriki katika operesheni ya kusomba mahindi kutoka kwa wakulima kipindi cha mwisho wa mwaka uliopita ili kunusuru mazao ya wakulima kuharibika
“Nawapongeza kwa umahili wenu kipindi cha oparesheni ya kusomba mahindi kutoka kwa wakulima kwani agizo nililotoa kwa makamanda wenu lilitekelezwa vyema” sasa wakulima wana nufaika na kazi mliyoifanya huo ndoi uzalendo alisisitiza mkuu wa Mkoa
Awali akitoa taarifa ya mafunzo kwa mkuu wa mkoa Kaimu kamanda kikosi cha 842 KJ Mlale Meja T S Mpupu  alisema mafunzo hayo ya awali ya kijeshi  yalianza tarehe 26 Julai 2011 na yanahitimishwa  tarehe 20 Januari 2012 lakini yatendelea hadi kipindi cha mkataba wa miaka miwili kitakapoisha
Aliongeza kusema wakati wanaanza kulikuwa na Vijana wapatao 827 kutoka katika mikoa yote ya Tanzania na wanapohitimu leo ni Vijana 822 kati yao wavulana ni 671 na wasichana ni 152
Aliendelea kueleza kuwa Vijana watano hawakuhitimu mafunzo kutokana na watatu kufariki dunia kwa matatizo ya ugonjwa na wawili walitoroka mafunzoni
Aidha kwa upande wake mwakililishi wa Mkuu wa Jeshi la kujenga Taifa Luteni Kanali Malembo aliwakumbusha wahitimu hao juu ya kiapo walichoapa mbele ya mgeni rasmi kuwa wataeendeleza utii  na kuitumikia nchi ya Tanzania kwa  uaminifu,utii na uhodari siku zote
Alisema kuwa watakapotoka hapo(Mlale) watasambazwa katika makambi mengine nchini ili wakaendelee na mafunzo ya stadi za uzalishaji hadi kipindi cha miaka miwili kitakapoisha hivyo aliwasihi kuwa na nidhamu
“Nidhamu ni kitu cha msingi unapokuwa Ndani ya Jeshi la Kujenga Taifa” alisema Luteni Kanali Malembo
Kikosi cha jeshi Mlale JKT kilianzishwa mwaka 1970 kikiwa na Malengo ya kuwalea Vijana  kwa kuwapatia mafunzo na stadi za uzalishaji mali ili wahitimipo waeze Aidha kuajiliwa na serikali au wajitegemee katika kuendeleza Uchumi wao na taifa.