Thursday, January 26, 2017

LAMI YA ST. DOMINIC YAKAMILIKA



Na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Halmashauri ya Manispaa ya Iringa imekalimisha ujenzi wa barabara ya St. Dominic kwa kiwango cha lami kwa zaidi ya shilingi 290,000,000.

Kauli hiyo ilitolewa na Kaimu Mhandisi wa Manispaa ya Iringa, Mhandisi Richard Moshi akiwasilisha taarifa ya utekelezaji kazi za matengenezo ya barabara kwa mwaka wa fedha 2015/2016 katika kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Iringa kilichofanyika katika ukumbi wa Chuo Kikuu cha Mkwawa mjini Iringa.

Mhandisi Moshi alisema kuwa katika mpango wa mwaka, upatikanaji wa huduma za miundombinu na mawasiliano kuboreshwa, ilipangwa kujenga barabara kwa kiwango cha lami barabara ya St. Dominic na kipande cha Ilala km 0.76 kwa kiwango cha lami. Alisema kuwa katika utekelezaji wa ujenzi huo, fedha iliyotengwa ni shilingi 348,614,279.40 wakati fedha iliyotumika ni shilingi 290,521,317.91 na mradi umekamilika na upo katika muda wa matazamio.   

Mhandisi Moshi alieleza ujenzi wa mifereji eneo la Mawelewele kata ya Mwangata km 2.3 na kuweka changarawe km 1.0 mtaa wa Kibarabara. “Utekelezaji wa mradi huu umefikia asilimia 85 kwa gharama ya shilingi 290,694,241” alisema Mhandisi Moshi.

Akiongelea matengenezo ya muda maalum ya barabara ya Makanyagio 1.5 km, shughuli iliyofanyika ni kuchimba mtaro na matengenezo hayo yamefikia asilimia 15. Aidha, fedha, zilizotengwa kwa matengenezo hayo ni shilingi 84,700,518.

Halmashauri ya Manispaa ya Iringa ina mtandao wa barabara zenye urefu wa km 525.969, kati ya barabara hizo, km 50.165 ni barabara kuu na barabara za Mkoa ambazo zinahudumiwa na Wakala wa barabara nchini (TANROADS) kwa matengenezo. Km 475.804 ni barabara zilizo chini ya mamlaka ya Manispaa na matengenezo yake hufanywa na Halmashauri ya Manispaa. Kati ya km 19.483 ni za lami, km 125.439 ni za changarawe na km 341.057 ni za udongo.
=30= 



No comments:

Post a Comment