Thursday, January 26, 2017

WALIMU, TUMIENI VIZURI ZANA



Na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Walimu wa elimu ya awali wa mikoa ya Iringa na Njombe wametakiwa kutumia vizuri mbinu za ufundishaji na kutoa nafasi kubwa kwa mtoto kujifunza.

Kauli hiyo ilitolewa na mwakilishi wa Afisa Elimu Mkoa wa Njombe, Stephen Bange alipokuwa akifunga mafunzo ya walimu wa elimu ya awali yaliyofanyika katika chuo cha ualimu Kleruu mjini Iringa jana.

Bange alisema “mtakapokwenda kufundisha hamna budi kutumia kwa usahihi mbinu za ufundishaji mlizojifunza na kuhakikisha kuwa mnatoa nafasi kubwa kwa mtoto kuweza kujifunza. Mbinu zote zitilie mkazo kwa mtoto kutumia mazingira halisi katika kujifunza. Mtoto apewe muda wa kufanya vitendo na majaribio yanayolingana na umri wake”. Aliongeza kuwa mtoto awezeshwe kutumia vitu halisi katika kujifunza. Mwalimu anapaswa kuandaa mazingira mazuri ya kujifunzia na kuandaa zana zenye mvuto na zinazokuza udadisi. 

Bange aliwataka walimu hao kuwashirikisha walimu ambao hawakushiriki mafunzo hayo, mambo yote waliyojifunza ili nao wawe mahili ikiwa ni pamoja na kutumia vifaa walivyotumia wakati wa mafunzo. 

Vilevile, aliwataka kutatua changamoto zinazojitokeza wakati wa ufundishaji na ujifunzaji ili kutekeleza mtaala wa elimu ya awali kwa ufanisi. 

Katika taarifa ya mafunzo iliyowasilishwa na Mratibu wa mafunzo, kutoka Taasisi ya Elimu Tanzania, Laurence Kunambi alisema kuwa taasisi ya elimu Tanzania imeboresha mitaala yote ya elimu msingi kutoka elimu ya awali mpaka darasa la sita. Taasisi imeshafanya maandalizi ya kuboresha mtaala wa elimu ya sekondari kidato cha kwanza hadi nne. Aliongeza kuwa TET imekwisha andaa vitabu vya kiada kuanzia elimu ya awali, darasa la kwanza hadi la sita pamoja na ngazi ya sekondari kidato cha kwanza hadi cha nne. Aliongeza kuwa kwa mara ya kwanza TET imeandaa vitabu vya kiada kwa kidato cha tano na sita.

Akiongelea mafunzo juu ya uboreshaji mtaala wa elimu ya awali yamefanyika kwa awamu nne, ambapo awamu ya kwanza yalihusisha wawezeshaji wa kitaifa 22. Awamu ya pili mafunzo yalihusisha wawezeshaji wa mikoa 375. Awamu ya tatu ambayo ndiyo hii inahusu mafunzo ya walimu wa elimu ya awali 16,129 katika vituo 18 nchi nzima.

Alisema kuwa katika mkoa wa Iringa na Njombe, walimu 957 watapatiwa mafunzo katika kituo cha chuo cha Kreluu.

Kunambi alisema kuwa mafunzo hayo yalilenga kuwajengea walimu wa elimu ya awali uwezo wa kutekeleza mtaala na muhtasari wa elimu ya awali ulioboreshwa wa mwaka 2016. Malengo mengine aliyataja kuwa ni kukuza uelewa wa dhana ya mtaala na muhtasari wa elimu ya awali na kumuwezesha mwalimu kutumia mtaala na muhtasari na vifaa vyake. 

Mengine ni kumuwezesha mwalimu kujenga uwezo wa kuhusisha kitabu na umahiri husika. Kubaini, kufaragua, kutengeneza na kutumia zana stahiki katika kufundisha na kujifunza na kumuwezesha mwlimu kujenga uwezo wa kufanya maandalizi sahihi ya ufundishaji.
=30=

No comments:

Post a Comment